Serikali imedhamiria kukabiliana na mafuriko yanayosababishwa na mvua kwa kujenga Mabwawa zaidi ya 10 yatakayogharimu zaidi ya shilingi Bilioni 50 yatakayotumika kukusanya maji ya mvua yanayotiririka kutoka Milimani ili yasilete athari kwa wananchi na kwenye miundombinu hususan ya usafirishaji na nyinginezo.
Hayo yamebainishwa na Waziri Mkuu wa Tanzania Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba alipokua akizungumza na wakazi wa Kata ya Gulwe, Wilaya ya Mpwapwa alipofanya ziara ya kikazi Januari 02, 2026, kukagua maeneo yaliyoathiriwa na mvua zinazoendelea kunyesha hususan miundombinu ya Reli.
“Serikali ya awamu ya sita ilipoingia madarakani ilianza ujenzi wa mabwawa kuanzia usawa wa Ruvu na Kidunda, tutajenga zaidi ya Mabwawa 10 ili kuelekeza na kuhifadhi maji yasilete mafuriko yaliyokua yakijitokeza, hivyo tumeshachukua hatua na hatua nyingine zinaendelea kukabiliana na masuala ya aina hii katika maeneo yanayohusisha Wilaya za Kilosa na Mpwapwa”.
Akitoa salamu za Mkoa, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Rosemary Senyamule amesema Mkoa wake ni miongoni mwa Mikoa inayoathirika na mvua lakini Serikali imeleta utatuzi wa muda mrefu kuepusha athari zaidi katika maeneo mbalimbali ya Wilaya za Mkoa huu na kubadirisha changamoto hizo kuwa fursa za kilimo.
“Kwa kipindi hiki maeneo mengi yamepatiwa utatuzi wa muda mrefu ambapo athari haziwezi kujirudia kwa kipindi kifupi hasa maeneo ya Mtanana (Kongwa), Fufu (Mpwapwa) na mengine mengi ambapo takribani shilingi Bilioni 64.3 zilitolewa kwa ajili ya kunusuru maeneo yanayoathirika na mafuriko”.
Vile vile, Mbunge wa Jimbo la Mpwapwa Mhe. George Malima, ameiomba Serikali kufikiria ujenzi wa Barabara kwa kiwango cha lami kutoka Mpwapwa Mjini hadi Gulwe kwenye kituo cha Reli ya mwendo kasi sambamba na kituo cha huduma za afya kwa ajili ya dharura za kiafya zinazoweza kujitokeza kutokana na uwepo wa stesheni hiyo.
Waziri Mkuu amefanya ziara hiyo ili kukagua athari zilizojitokeza kwenye miundombinu ya Reli ya mwendo kasi (SGR) kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha msimu huu ambapo ameanzia katika Mikoa ya Dar es salaam, Morogoro na Dodoma ambayo inapitiwa na Reli hiyo







Mpwapwa - Dodoma, Tanzania
Anwani: S.L.P 12
Simu: 255 26 2320122/2320
Simu ya Kiganjani: 0684705551
Barua pepe: info@mpwapwadc.go.tz
Copyright © 2021 Mpwapwa District Council . All rights reserved.